Togo:#coronavirus:Janga linaweza kuwa fursa ya uongofu wa binadamu!
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican
Mlipuko wa virusi vya corona unaleta wasiwasi mkubwa kwa binadamu lakini unaweza hata kuwa fursa ya uongofu wa kumkaribia Mungu. Amethibitisha hayo Askofu Mkuu Nicodéme Anani Barrigah wa jimbo Kuu Katoliki la Lomé, nchini Togo kupitia Tovuti ya Baraza la Maaskofu wa Kanda ya Afrika Magharibi (Recowa-Cerao). “Virusi vya corona licha ya tishio na ubaya wake ni fursa kwa ajili ya kufikiria kwa upya namna yetu ya kuishi ili kurudia tena kwa upya Mungu kwa kujipatanisha naye na jirani. Tusipoteze fursa hii kwa sababu Bwana kwa njia ya matukio kama haya anazungumza pamoja nasi”, amesisitiza Askofu Mkuu Barrigah.
Fuateni kanuni na taratibu zilizowekwa na serikali na Kanisa
Kwa muktadha huo, Askofu Mkuu anawashauri waamini wote kuheshimu kanuni za afya ili kuweza kuzuia maambukizi zaidi na kufafanua juu ya umuhimu wa uwajibikaji kwa kila mmoja katika kutunza afya binafsi na ile ya jirani. Hata hivyo wito wa nguvu wa askofu Mkuu ni katika sala kwa sababu anamesema, kusitisha misa katika makanisa kimwili haina maana ya kusitisha sala kiroho kwa waamini wote na hivyo amewaalika kusali zaidi katika kipindi hiki kwa maana "milango ya Kanisa umefungwa, japokuwa imefunguliwa milango wazi ya mioyo".
Tusipoteze matumaini au kuogopa
Askofu Mkuu anasema, “imani ni muhimu kwa maana sala kwa Bwana inatusaidia na kuwa nguzo, inatutia moyo ili tusipoteze matumani au kuogopa na kuchanganyikiwa; inatuangazia na kuwaangazia awali ya yote walioko wako msitari wa mbele dhidi ya virusi vya corona, kama madaktari, wauguzi, wahudumu wa afya wote na pia wale ambao wanapaswa kuchukua uamuzi na hatua zote za utekelezaji.