Seminari Ndogo ya Mtakatifu Petro, Jimbo Katoliki la Morogoro inaadhimisha Jubilei ya Miaka 50 tangu kuanzishwa kwake! Matendo makuu ya Mungu! Seminari Ndogo ya Mtakatifu Petro, Jimbo Katoliki la Morogoro inaadhimisha Jubilei ya Miaka 50 tangu kuanzishwa kwake! Matendo makuu ya Mungu! 

Jubilei ya Miaka 50 ya Seminari ya Mtakatifu Petro Morogoro! Kumekucha!

Seminari Ndogo ya Mtakatifu Petro, Jimbo Katoliki la Morogoro inaadhimisha Jubilei ya Miaka 50 tangu kuanzishwa kwake mwezi Agosti 1969 kama sehemu ya utekelezaji wa Agizo la Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania la Mwaka 1967: Hapa ni mahali pa kulea miito, kwa kukazia tunu msingi za maisha ya Kikristo na ukomavu wa: kiakili, kiroho, kiutu na kimaadili. SPS kitovu cha elimu.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Hivi karibuni, Baraza la Kipapa kwa ajili ya Wakleri limechapisha mwongozo wa malezi ya Kipadre unaojulikana kama “Ratio Fundamentalisi Institutionis Sacerdotalis” yaani “Zawadi ya wito wa Kipadre”. Utangulizi wa mwongozo huu unabainisha changamoto iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko kama sehemu ya mchakato wa kulinda, kukuza na kudumisha wito na maisha ya Daraja Takatifu ya Upadre. Huu ni wito wenye thamani kubwa katika maisha na utume wa Kanisa unaopaswa kuhudumiwa kwa umakini mkubwa kwa kuheshimu dhamiri nyofu, wajibu unaotekelezwa kwa unyenyekevu na uvumilivu mkubwa, ili kweli Wakleri waweze kung’ara kati ya watu wa Mungu wanaowahudumia!

Mwongozo huu ni matunda ya ushirikiano mkubwa kutoka katika Sektretarieti kuu ya Vatican, kazi iliyoanza kutimua vumbi kunako mwaka 2014. Mwongozo unatoa kwa muhtasari sheria, kanuni na mambo msingi ambayo yanapaswa kuzingatiwa kwa ajili ya malezi na makuzi ya wito wa Daraja Takatifu ya Upadre. Unabainisha wajibu wa Mabaraza ya Maaskofu Katoliki; Waratibu wa Seminari kitaifa na kimataifa pamoja na mwongozo wa malezi ya Seminari moja moja. Mwongozo huu unapembua kwa kina na mapana kanuni msingi za maisha na wito wa Daraja Takatifu ya Upadre: Yaani wanapaswa kuunganika na Kristo ili kuwaongoza, kuwachunga na kuwatakatifuza watu wa Mungu. Wanapaswa kuungana na Kristo Yesu katika maisha, upendo na ukweli kwa ajili ya wokovu wa watu na kuendelea kuwa ni mwanga wa mataifa na chumvi ya dunia. Dhamana ya Kanisa ni kulea, kusindikiza na kupalilia miito mitakatifu, lakini kwa namna ya pekee wito wa Daraja Takatifu.

Seminari ndogo na nyumba za malezi ni mahali pa kulea na kuwasindikiza vijana katika maisha na wito wa Daraja Takatifu ya Upadre. Hapa waseminari wadogo wanapaswa kupewa malezi ya tunu msingi za maisha ya Kikristo kwa kukazia majiundo ya kiakili, kiroho, kiutu na kimaadili. Ni mahali pa kukuza ukomavu, umoja na mshikamano na Kristo Yesu kwa njia ya Sala, Neno la Mungu na Mashauri ya Kiinjili. Walezi wawe kweli ni mashuhuda wa Injili ya Kristo! Mwongozo pia unaangalia wito kwa Daraja takatifu wa watu wenye umri mkubwa, wasaidiwe na kupatiwa malezi makini katika nyumba maalum, ili waweze hatimaye, kufanya maamuzi muhimu katika maisha yao! Waseminari ni matumaini ya Kanisa katika ujumla wake. Ni katika muktadha huu,  Seminari Ndogo ya Mtakatifu Petro, Jimbo Katoliki la Morogoro, Ijumaa tarehe 21 Februari 2020 inazindua maadhimisho ya Jubilei ya Miaka 50 tangu kuanzishwa kwake; kwa Ibada ya Misa Takatifu inayotarajiwa kuongozwa na Askofu Agapiti Ndorobo wa Jimbo Katoliki la Mahenge ambaye pia tunda la Seminari Ndogo ya Mtakatifu Petro, Jimbo Katoliki la Morogoro.

Mgeni rasmi katika maadhimisho haya ni Jaji Mstaafu Bernard Luanda ambaye pia ni tunda la Mama “SPS” kama anavyojulikana kwa wale wote waliochota hekima, ujuzi na maarifa kutoka kwake! Kati ya mambo msingi yanayofanyika katika uzinduzi wa Jubilei ya Miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Seminari Ndogo ya Mtakatifu Petro Morogoro ni harambee ya kuchangia ukarabati mkubwa wa miundo mbinu, ili kukabiliana na changamoto mamboleo pamoja na kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia, ili kweli Kanisa na jamii iweze kupata viongozi makini, watakatifu na wachapakazi. Jimbo  la  Morogoro  lina  seminari  ndogo  moja  ambayo  inamilikiwa  na  Majimbo  ya  Morogoro,  Jimbo kuu la Dodoma,  Tanga,  Same,  Zanzibar  na  Jimbo  kuu  la  Dar  es  Salaam. Kuunda  seminari  moja  ya  majimbo  ni  uamuzi  uliotokana  na  Kikao  cha  Maaskofu  Katoliki  Tanzania   cha  mwaka  1967.  Seminari ya Mtakatifu Petro, Morogoro ilijengwa ili kutekeleza azimio  hilo. Seminari ya Mtakatifu Petro ambayo  historia  yake  inaanza  huko  Ilonga  katika  mwaka  wa  1937,  na  kuhamia  baadaye  Bagamoyo  mwaka 1939  ina  vidato  I  hadi  VI.  Seminari inaongozwa na Bodi ya Magavana ambayo ni Maskofu wa majimbo yanayohusika.  Kwa maswala madogo madogo Maaskofu huwakilishwa  na  wakurugenzi  wa  miito  wa  majimbo  yanayohusika.

Ingawaje mpango wa kuwa na seminari ya jumla pia ilikuwa  na  manufaa  yake,  lakini  majimbo  yaliyotajwa  hapo  juu  sasa  kila  moja  ina  seminari  yake  ya  jimbo  isipokuwa  jimbo  la  Zanzibar.  Mpaka Mei, 1992 kumekuwa  na  waseminari  258  ambao  kati  yao  213  wako  katika  vidato I – VI  na  45  wapo  vidato  V – VI.  Wanafunzi hao wanatoka majimbo mbalimbali na Mashirika ya kitawa na kazi za kitume kutoka sehemu mbali mbali za Tanzania.  Majimbo hayo ni: Singida (1); Morogoro (107); Mahenge (3); Jimbo kuu la Dodoma (37); Zanzibar (16); Jimbo kuu la Mbeya (1); Lindi (2); Moshi (5); Tanga (5); Rulenge (1); pamoja na Majimbo  Makuu  ya  Dar  es  Salaam (59);  Songea (2)  na  Mwanza (1). Mashirika yenye waseminaristi ni Wakarmeliti (14); Wastigmatine (1). Seminari Ndogo ya Mtakatifu Petro Morogoro ilifunguliwa rasmi mwezi Agosti 1969 na Mwadhama Kardinali Laurean  Rugambwa.  Magambera kadhaa wameshaiongoza seminari ya Mtakatifu Petro. 

Seminari hii kwa namna ya pekee inamkumbuka kwa  masikitiko  Gambera  wa  kwanza  hayati  Padri  Nicas  Kipengele  ambaye  baadaye  alikuwa  Askofu  wa Jimbo Katoliki la  Mahenge (1970 – 1971). Wengine  ni  Mapadri  Emmanuel  Makala  wa  Morogoro;  Martin  Maganga  wa  Tanga;  Damas  Mpunta  wa  Dodoma  (1974 – 1979),  Octavian  Linuma  wa  Mahenge  (1980 – Agosti  1987) Wengine ni  Padre Bunus  Kizee  wa  Mahenge; Padre Patrick Kung’aro, Jimbo Katoliki la Morogoro, Padre M. Chikila, Padre Joseph Mluge, Jimbo Katoliki la Morogoro, Padre Karoli Mloka, Jimbo Katoliki Morogoro, Padre Valentini Chilega, Jimbo Katoliki Morogoro na kwa sasa Padre Aloyce Mwenyasi wa Jimbo Katoliki Morogoro.

Seminari ya Mtakatifu Petro Morogoro imewahi kushika nafasi ya kwanza katika kufaulu mtihani wa  kidato  cha  nne  wa  mwaka 1990 kitaifa. Seminari ndogo ya Mtakatifu Petro iliyopo Jimboni Morogoro ni shule inayomilikiwa na Kanisa Katoliki  inayotoa  elimu  ya  sekondari  kufikia  kidato  cha  sita. Pia shule hii, inafundisha malezi  maalumu  ya  Kikristo  na  maadili  kwa  vijana  wanaoandaliwa  kuwa  mapadre  wa  Kanisa Katoliki. Shule hii inamilikiwa  kwa  pamoja  na  majimbo  saba  ya  Kanisa  Katoliki,  yaani  Dar  es  Salaam,  Zanzibar,  Morogoro,  Tanga,  Same,  Mahenge,  Kwa  ruhusa  maalumu  ya  Mwenyekiti  wa Bodi  ya Maaskofu, Seminari hiyo  ina  wanafunzi  wanaojulikana  kama  waseminaristi  kutoka jimbo kuu  la  Songea, mashirika  ya  Wasalvatori, Wabenediktine na  Wakarmeli.

Kihistoria Seminari hii ilianzia Ilonga,Wilayani  Kilosa, Mkoani Morogoro  mwaka  1936, Kisha  ikahamia  Bagamoyo  na 1969  ikahamishiwa  Morogoro  ilipo  hadi sasa. Utume wa seminari hiyo maarufu kwa jina la “Saint Peter’s  Seminary”  tangu iasisiwe  ni  kutoa  elimu  bora  na  malezi  bora  kwa  vijana  wenye mwelekeo  wa  kuwa  mapadre  kwa gharama  nafuu  ambayo  hata  familia  zenye  kipato  kidogo wanaweza  kuimudu. Gambera Msaidizi wa seminari hiyo, Padre Joseph Torondo anasema seminari hiyo ni moja ya shule  zenye  kiwango  kidogo  cha ada  miongoni  mwa  shule  za  bweni  za  kulipia  nchini Tanzania Seminari hii imekuwa na mafanikio makubwa  katika  nyanja  mbalimbali  hususani  katika  kutoa wahitimu  wengi  wakiwamo  mapadre, maaskofu  na viongozi  wengine  wa  serikali  na  taasisi  binafsi. Historia inaonesha kuwa Seminari Ndogo ya Mtakatifu Petro, ni moja kati ya shule bora Tanzania kwa wanafunzi kufanya vizuri katika mitihani  yao  ya  Taifa.Pamoja  na  ukweli  kuwa  kuna  nyakati  inashuka,  lakini  daima kiwango  cha  taaluma ni kizuri. Padre Torondo anasema wale ambao hawakufikia lengo la kuwa mapadre wamekuwa hazina njema kwa jamii  ndani  na  nje  ya  Tanzania.

Baadhi ya Maskofu waliosoma katika Seminari Ndogo ya Mtakatifu Petro Morogoro ni: Askofu Agapiti Ndorobo wa Jimbo  Katoliki  la  Mahenge, Askofu mstaafu Jacob  Koda wa Jimbo Katoliki la Same, Askofu  Msaidizi  Eusebius Nzigilwa Jimbo kuu  la  Dar  es  Salaam, Askofu Titus Mdoe wa Jimbo Katoliki la Mtwara pamoja  na  Askofu  Bernardine  Mfumbusa wa  Jimbo Katoliki  la Kondoa. Mbali na  viongozi  hao wa  dini, pia  kuna  viongozi   wa  Serikali waliosoma  katika  shule hii  akiwamo  Jaji  wa  Mahakama  ya Rufaa, Bernard Luanda, aliyekuwa  Katibu  wa  Rais mstaafu Jakaya Mrisho  Kikwete, Prosper  Mbena  ambaye  kwa  sasa  ni  Mbunge, aliyekuwa  Mkurugenzi  wa Mpango  wa Shirika  la  Taifa  la Hifadhi  ya  Jamii  (NSSF),Crescentius  Magori. “Kwa ujumla ni kwamba Seminari yetu imetoa  wataalamu  katika  medani  mbalimbali  wakiwamo  walimu, wanahabari, wanadiplomasia, wanasheria, waandishi  na  wanauchumi” Anasema  Padre  Torondo. Kuna Mapadre waliohitimu Seminarini hapo na wanaendelea kutoa mchango mkubwa katika maisha na utume wa Kanisa la Kiulimwengu. Monsinyo Romanus Mbena, Mshauri mkuu wa Ubalozi wa Vatican nchini Albania. Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S, Shirika la Wamisionari wa Damu Azizi ya Yesu, anatekeleza utume wake Radio Vatican, huko mjini Vatican. Kuna wengine wengi ambao wanaendelea kuchakarika sehemu mbali mbali za dunia kama wamisionari, matunda ya Seminari Ndogo ya Mtakatifu Petro.

Kung’ara: Miaka  ya  1990  seminari  hii  ilikuwa  miongoni  mwa  shule  bora  nchini Tanzania  kutokana  na  kushika  nafasi  za  juu  kitaifa  kidato  cha  nne,  ambapo  mwaka  huo,  Seminari  ndogo  ya  Mtakatifu Petro  Morogoro  ilishika nafasi  ya  kwanza  kitaifa  kati  ya  shule  305,  na  mwaka  1992  ikashika  tena  nafasi  ya  kwanza  kitaifa. Mwaka 1996 ilishika nafasi ya 13 kati  ya  shule  506  kitaifa  na  1998,  ikashika  nafasi  13  kati  ya  shule  611  kitaifa.  Mwaka 2000 ilikuwa ya nane kati  ya  shule  611  za  sekondari  kitaifa  kidato  cha  nne. Mwaka 2001, ilishika nafasi  ya  saba  kati  ya  shule  619  kitaifa.  Baada  ya  kiwango  cha  ufaulu  katika  shule  hii  kilianza  kuporomoka  kwani  mwaka  2003  ilishika  nafasi  ya  23  kati  ya  shule  754  kitaifa  hali  ambayo  haikuwapendeza  viongozi  wa  shule. Kwa mwaka 2012 idadi ya  watahiniwa  ilikuwa  60  waliopata  daraja  la  kwanza  walikuwa  watatu,  daraja  la  pili  15,  daraja  la  tatu  19,  daraja  la  nne  23,  shule  ikashika  nafasi  67  kati  ya  3,392  kitaifa.

Mwaka 2013 idadi ya watahiniwa ilikuwa ni 30 waliopata  daraja  la  kwanza  walikuwa  ni  watatu,  daraja  la  pili  tisa,  daraja  la  tatu  17  na  mwanafunzi  mmoja  alipata  daraja  la  nne  shule  ilishika  nafasi  ya  48  kati  ya  1,099  kitaifa. 2015 idadi ya  wahitimu  ilikuwa  ni  45  waliopata  daraja  la  kwanza  walikuwa  21,  daraja  la  pili  walikuwa  wanafunzi  33,  daraja  la  tatu  mmoja  ambapo  shule  hii  ilionekana  kufanya  vibaya  zaidi  kwani  ilishika  nafasi  ya  77  kati  ya  shule  3,452  kitaifa. Kwa kidato cha sita, mwaka 1988 idadi ya watahiniwa ilikuwa ni 13, waliopata  daraja  la  kwanza  walikuwa  ni  wanafunzi  tisa,  daraja  la  pili  wane.  Shule hiyo ikashika nafasi ya kwanza kitaifa kati ya shule 75. Aidha, mwaka 1989 idadi ya wanafunzi ilikuwa 38 waliopata daraja la kwanza walikuwa  wananfunzi  10,  daraja  la  pili  14,  daraja  la  tatu  12,  daraja  la  nne  mmoja  na  sifuri  mmoja.  Mwaka huo shule  ilishika  nafasi  ya  18  kati  ya  shule  70  kitaifa. Mwaka 1990 ilikuwa na  watahiniwa  21,  waliopata  daraja  la  kwanza  walikuwa  saba,  daraja  la  pili  10,  daraja  la  tatu  wane.  Shule hiyo ikashika  namba  9  kati  ya  shule  75  kitaifa.

Mwaka 2010 ilikuwa na wanafunzi 25 waliopata  daraja  la  kwanza  walikuwa  wanne,  daraja  la  pili  15,  daraja  la  tatu  16.  Shule ikashika  nafasi  ya  nane  kati  ya  shule  81  kitaifa. Aidha, 2011 kulikuwa na watahiniwa 51.  Waliopata daraja la kwanza walikuwa 10, daraja la pili 23, daraja la tatu 17 na mmoja  alipata  daraja  la  nne,  hivyo  shule  ikashika  nafasi  ya  29  kati  ya  shule  334  kitaifa. Mwaka 2012 watahiniwa  walikuwa  37.  Wahitimu saba wakapata  daraja  la  kwanza,  darja  la  pili  walikuwa  17,  10  daraja  la  tatu,  watatu  wakapata  daraja  la  nne,  shule  ikashika  namba  36  kati  ya  shule  326  kitaifa. Mwaka uliofuata kulikuwa  na  watahiniwa  17,  wanafunzi  9  wakapata  daraja  la  pili,  daraja  la  tatu  walikuwa  nane,  shule  ikashika  nafasi  ya  9  kati  ya  shule  121  kitaifa  na  ya  kwanza  kimkoa  kati  ya  shule  7  kwa  shule  zenye  wanafunzi  chini  ya  30. Aidha, mwaka 2014 idadi ya wanafunzi ilikuwa 31.  Waliopata daraja la kwanza mmoja, la pili 12, la tatu 18 Seminari hiyo ikawa namba 119 kati ya shule 268 kitaifa. Mwaka 2019 watahiniwa walikuwa 31, mmoja alipata daraja la kwanza, la pili 20 na daraja la tatu 10, shule  ikashika  nafasi  ya  137  kati  ya  shule  423  kitaifa.

Changamoto: Pamoja na nia nzuri ya seminari hiyo ambayo kwa  sasa  ina  wanafunzi  290,  ni  kutoa  elimu  na  malezi  bora  kwa  gharama  nafuu,  shule  imejikuta  katika  wakati  mgumu  kiuchumi.  Bajeti ya shule inakuwa ndogo na hivyo kuathiri mambo mengi. Na kwamba kupungua kasi ya ufaulu tofauti na miaka ya nyuma kumechangiwa  na  changamoto  kadhaa  zilizopo  shuleni  hapo  ambazo  baadhi  yake  zimesababishwa  na  uhaba  wa  fedha. Baadhi ya changamoto hizo kuwa ni uchakavu wa miundo mbinu, uhaba wa  vitabu  vya  kiada  na  rejea  kwa  matumizi  ya  wanafunzi,  uhaba  mkubwa  wa  vifaa  vya  maabara  ikiwa  ni  pamoja  na  shule  kutokuwa  na  uzio.

Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa Watu ambalo kwa miaka mingi lilikuwa linatoa ruzuku kwa ajili ya kusaidia kupunguza makali ya uendeshaji wa Seminari, imesitisha ruzuku. Mwamko kwa wakati huu ni waamini kuanza kuyategemeza Makanisa mahalia kwa rasilimali watu na vitu. Inakatisha tamaa kuona kwamba, waseminari wengi wanaishia njiani bila ya kuendelea na wito wa Upadre, tofauti na miaka ya  nyuma,  ambapo  takribani  robo  tatu  ya  wahitimu  walikuwa  wanafikia  Daraja Takatifu ya Upadre. “Kati  ya  wahitimu  30  wanaoendelea  na  masomo  ya  juu  ngazi  ya  seminari  huwa  mmoja  au  wawili,  kimsingi  hali  hii  inasikitisha  ndio  maana  wafadhili  wakachukua  uamuzi  wa  kusitisha  utoaji  msaada,”  anasema  Padre  Torondo  ambaye  pia  amesoma  seminarini hapo!

Mpango mkakati: Kwa sasa Seminari imekamilisha ujenzi wa madarasa mapya mawili  kwa  ajili  ya  wanafunzi  wa  kidato  cha  tano  na  sita  mchepuo  wa  sayansi na tayari yameanza kutumika na wanafunzi wake wako kidato cha sita kwa mwaka 2020. Pia uongozi umedhamiria kujenga maabara mpya na kuongeza vitatu kwenye maktaba  hatua  ambayo  itasaidia  kurejesha  ufaulu  mzuri  kwa  wanafunzi. “Tumedhamiria kuboresha mradi wa mifugo hususani nguruwe, ng’ombe wa maziwa pamoja na kuku ili kuongeza kipato na kuboresha lishe ya majandokasisi. “Tunaamini tukiwa na uchumi imara seminari yetu itakuwa katika nafasi ya kuendelea na utume wake wa kutoa elimu bora ya  sekondari na  malezi  bora  kwa  vijana  wenye  muelekeo  wa  kuwa  mapadre  kwa  gharama  nafuu  inayoweza  kulipwa  hata  na  familia  zenye  kipato  cha  chini,”  anasema Padre  Torondo.  Mwito wake kwa wahitimu waliosoma shuleni hapo ni kujitokeza kuisaidia kwa namna  yoyote  ile.

“Wakati uongozi wa seminari unabuni na kutekeleza  miradi  ya  kiuchumi,  ni  muhimu  pia  kuomba  wahisani  ndani  na  nje,  mashirika,  vikundi  na  mtu  mmoja  mmoja  ambao  wanaamini  katika  utume  wa  seminari  hii  ili  waungane  nasi  katika kuchangia maendeleo ya  utume  huu,”  anasema. “Tunawashukuru sana wanafunzi waliosoma hapa zamani (St. Peter’s Seminary Alumni) ambao kwa namna ya pekee hivi karibuni wameamua kusaidia maendeleo ya seminari hii, naomba wasichoke waendelee kuisaidia.” Mabweni matano yaliyopo shuleni hapo yamepewa majina ya mashahidi wafia dini wa Uganda.  Mabweni hayo ni pamoja na bweni la Kagwa, Tuzinde, Mukasa, Mulumba na  Kizito.

Miaka 50 ya St. Peter's Morogoro
20 February 2020, 14:10