Lugha za asili bado ni muhimu kwa mustakabali wa ulimwengu!
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican
Lugha za asili bado ni muhimu kwa mustakabali wa ulimwengu hivyo tufanye kila namna kuzitunza. Hii ni moja ya kauli alizozitoa rais wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa Tijjani Muhammad Bande katika mkutano wa ngazi za juu wa kuhitimisha mwaka wa kimataifa wa lugha za asili uliofanyika tarehe 17 Desemba 2019 katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa mjini New York Marekani.
Katika kauli yake Bande amesema juhudi ambazo zimefanyika ni pamoja na uundwaji wa Jukwaa la kudumu la watu wa asili. Pia Umoja wa Mataifa umekuwa chombo kikuu cha kukuza ufahamu kuhusu lugha za asili, na pia hatua zinazotakiwa kuchukuliwa ili kuzuia kutoweka kwa kwake. Akiendelea amsema :“Tukirejea kuanzia mwaka 1982, Umoja wa Mataifa ulianzisha kundi kazi kuhusu watu wa jamii ya asili. Pia mwaka wa kimataifa wa 2019 wa lugha za asili ni ushahidi tosha wa uwajibikaji wa Umoja wa Mataifa katika kuhifadhi lugha zilizoko hatarini.”
Je Takwimu zinasemaje? Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa, kila wiki mbili, takribani lugha moja ya asili inatoweka na hivyo kufaanya takribani lugha mbili za asili kutoweka kila mwezi. Lugha za asili 4,000 zilizosalia zinazungumzwa na asilimia 6 tu ya watu wote duniani.
Katika kutoa ushauri Balozi Bande ameeleza kuwa ana matumaini hali itakuwa sawa ikiwa taasisi za kielimu, sekta binafsi na wadau wa jamii awatachukua hatua za kuhakikisha wanaweka njia za kuzuia lugha za asili kupotea. Pia ameshauri shule kuchangia kwa kiasi kikubwa katika utunzaji wa lugha za asili kwa kuziingiza katika mitaala huku jamii ya asili mayo ikiona kuwa utunzaji wa lugha za asili ni utunzaji wa historia zao na vile vile ndimo maono ya kisayansi yanapo tunzwa, busara na shughuli za jamii zinazosogeza mbele jamii kutoka hatua moja kwenda nyingine.