KENYA:Kanisa barani Afrika litunze thamani za jumuiya na umoja!
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican
Balozi wa Vatican nchini Kenya na Sudan Kusini Askofu Mkuu Hubertus Matheus Maria van MEGEN, ametia moyo Kanisa la Afrika la kuendelea kutunza thamani za kijumuiya za kiafrika na umoja katika shughuli za kijamii. Amesema hayo alipotembelea katika Ofisi ya Sekretarieti ya Jumuiya ya Baraza la Maaskofu Afrika Mashariki (AMECEA), tarehe 3 Septemba 2019 jijini Nairobi. Askofu Mkuu van Megen amesema waafrika wanapaswa wandelee kukumbatia umoja na kukana hatari za ubaperi, ubinafsi wa ubepari wa nguvu na mengine mengi ambayo amesisitiza kwamba yamechangia ukosefu wa haki na ukosefu wa thamani za maisha ya binadamu katika sehemu nyingi za ulimwenguni.
Waafrika wana zawadi nzuri sana ambayo hawapaswi kuipoteza. Iwapo wataipoteza watakuwa na mwelekeo sawa na nchi za Magharibi,ambapo ndiyo unakuwa mwisho wa jamii inayofanya kazi, amesema Askofu Mkuu Van Megen. Aidha ameongeza kuwa, jamii inaweza kufanya kazi tu wakati kuna hisia za ushirikiano na ambayo inazidi kupungua katika jamii za Magharibi. Katika nchi hizo, watu hawachukui jukumu zaidi katika ngazi ya serikali hata katika ngazi ya familia. Watu hawajali wengine, hata watoto wao wenyewe,” amesisitiza Balozi wa kitume. Kadhalika akiendelea kusisitiza zaidi amewametia moyo Makanisa ya Afrika kuanzisha utamaduni wa ushirikiano na nchi ambazo zimepoteza hisia za kuthamini pia ameongeza kusema kuwa:“licha ya changamoto zote ambazo Afrika inakabiliana nazo kama vile ufisadi, mzigo wa magonjwa, vita, umasikini na mengine mengi, waafrika bado wanao ufahamu wa dhati wa thamani ya maisha ya mwanadamu”.
Hata hivyo Askofu Mkuu Van Megen pia ameweza kuchangamotisha AMECEA ili kujikita kwa kina katika kuimarisha Kanisa ili liweze kuwa jiwe hai, na siyo tu kupitia ujenzi wa miundombinu. Katika hili Askofu Mkuu amesema, wao tayari ni Kanisa la Miundo, japokuwa wakati mwingine kuna tabia ya kusema, ikiwa tunayo miundo mahali, basi kila kitu ni sawa. Lakini kumbe anamnukuu Baba Mtakatifu kwamba anakumbusha kuwa muundo unahitaji kuwa jiwe hai. “Kanisa limeundwa na mawe yaliyo hai mahali ambapo kila mtu anachangia maisha yake na kila jumuiya katika kujikita kwa dhati kwenye ujenzi wa kazi ya Kanisa”. Aidha amewakumbusha pia jinsi gani Baba Mtakatifu Francisko anasisitiza kuwa hawataweza kuokoa Kanisa kupitia miundo mbinu; Lakini kumbe inawezekana kuokoa Ukristo tu kwa kuhakikisha kuwa mwili wa Kristo upo na unaendelea kukua na kustawi katika jamii kupitia njia ya kujitolea binafsi. Kwa upande wake, Askofu Mkuu pia amethamini kazi ambayo imefanywa ya kujitolea na inayoonyeshwa na AMECEA huku akizingatia kwamba ubora upo, kujitolea na mchango muhimu kwa Kanisa huko Afrika.
Na kwa niaba ya AMECEA, kupitia Katibu Mkuu wake, Padre Anthony Makunde, na Mratibu wa wakichungaji pia Naibu Katibu Mkuu wa masuala ya kichungaji, Padre Emmanuel Chimombo wameelezea kuhusu AMECEA inavyojikita kwa undani kulinda utakatifu wa maisha ya mwanadamu na kusisitizia kuwa maisha ya mwanadamu huanzia wakati wa kutungwa kwake hadi kifo cha asili, na kwa maana hiyo AMECEA imechukulia suala la ulinzi wa watoto kwa umakini zaidi. Vile vile Balozi wa kitume katika ziara hiyo amepata kukutana na wanafanyakazi wote wa AMECEA ambao walijitambulisha katika idara zao, wakielezea kile wanachofanya, kabla ya kuwa na mkutano wake na wafanyakazi wote ndani ya sekretarieti ya AMECEA.