Malawi:Mshikamano wa Maaskofu kwa waathirika wa mafuriko!
Na Sr. Angela Rwezaula - Vatican
Wakati wa ziara ya kuwatembelea waathirika wa Kimbunga Idai inchini Malawi, Askofu Mkuu Thomas Luke Msusa, wa Jimbo Kuu la Blantyre na Rais wa Baraza la Maaskofu katoliki nchini Malawi (ECM), akiwa na wawakilishi wa Baraza hilo amesema, “tuko hapa kwa ajili ya kuleta mshikamano wetu kwa ajili yenu na kutimiza uwajibikaji wetu wa kusaidia mwenye kuhitaji. Akizungumza na watu waliojikusanyika katika makambi yaliyojaa sana ya Makina, Matiya na Mwalija, Askofu Mkuu Msusa amesema: “Maaskofu wanaelewa matatizo ambayo mnapitia. Na kwa maana hiyo, tumeomba wadau wa Kitengo cha maendeleo fungamani ya watu Katoliki,msaada kutoka Shirika la Kipapa la Kanisa Hitaji, Cordaid, Sign of Hope, Caritas ya Australia na Caritas ya Korea, kupitia Caritas Internationalis ili kutusaidia kwa ajili ya kuweza kuwasaidia ninyi".
Shukrani kwa msaada wa mashirika mbali mbali katoliki duniani
Askofu mkuu Msusa aidha ameongeza kusema:“Tunawashukuru kwa msaada wao kwa ajili yenu na tunaweza kutatua baadhi ya matatizo yenu". Pongezi pia hata kwa rasilimali ambazo tayari zipo, na ambapo Baraza la Maaskofu kwa njia ya Tume ya maendeleo katoliki (CADECOM), watajenga nyumba 450, katika maeneo matatu yaliyo athirika zaidi ya Zomba, Chikwawa na Phalombe. Mpango huo unatazamia hata utoaji wa maji salama ya kunywa kwa kutengeneza visima. Mafuriko yalisababisha waathirika wa vifo 57 nchini Malawi na milioni moja kubaki bila makazi na nusu yao wakiwa ni watoto katika wilaya kumi na nne. (Fides 13/4/2019)