Tafuta

Utukufu wa Kristo Yesu umetundikwa juu ya Msalaba! Utukufu wa Kristo Yesu umetundikwa juu ya Msalaba! 

Utukufu umetundikwa katika Fumbo la Msalaba!

Utukufu wa Kristo Yesu umetundikwa juu ya Msalaba, kielelezo cha hali ya juu kabisa cha unyenyekevu unaokoa! Uongozi kadiri ya Maandiko Matakatifu ni huduma kwa watu wa Mungu, hasa maskini na wale wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii!

Na Padre Joseph Peter Mosha. – Vatican.

Mwanadamu anapotenda jambo au huduma kwa jamii hutegemea kupata mrejesho fulani kutokana na huduma yake. Mrejesho huu unaweza kutoka kwa wale anaowafanyia huduma hiyo au kwa yule anayemtuma. Mmoja atapenda kupata shukrani, kupokea sifa na pongezi na zaidi kutuzwa kwa sababu ya huduma yake. Katika hali ya kawaida hili linaonekana kuwa ni haki lakini haki hii mara nyingi hutupeleka katika hatari iliyofichika. Mmoja anapokosa matarajio hayo ya moyo wake ni rahisi sana kuongozwa na ubinafsi wake na mwishowe kunakuwa na hatari ya kuharibu au kuzorotesha au kuyapindua makusudi ya huduma anayotarajiwa kuifanya.

Dominika ya leo inatupatia fursa ya kujitafakari nafsi zetu na pengine kuiepuka hatari hiyo. Tunakumbushwa leo juu ya gharama ya ufuasi wetu: ni kumtumikia Mungu ambaye anatuita kuwa uaminifu kwake. Ni mwaliko wa kuitikia wito huo wa Mungu na tuzo yetu tuionje katika uwepo wake ndani mwetu na ndani ya wenzetu. Bwana wetu Yesu Kristo anakuwa kwetu ni kielelezo kama anavyoaguliwa katika somo la kwanza na Nabii Isaya katika mfano wa mtumishi wa Bwana. “Bwana aliridhika kumchubua…” Hivi ndivyo anavyoelezewa huyu mtumishi wa Bwana anayetumwa kuutangaza na kuudhihirisha wokovu wa Mungu. “Bwana aliridhika kumchubua; amemhuzunusha”. Anoneshwa katika hali ya mateso na huzuni; anaitwa kutumikia lakini anawekwa katika hali ya kupokea mateso na huzuni.

Ingawa anatoka kwa Mungu, na yeye mwenyewe ni Mungu anatumwa katika namna inayoonesha mapinduzi makubwa katika matarajio ya kibinadamu. Kwake Yeye muhimu ni kuutekeleza mpango wa Mungu kwani “mapenzi wa Bwana yatafanikiwa mkononi mwake”. Sehemu hii inatuonesha tabia muhimu katika wito wa kuitikia utumishi wa Mungu; si katika malipo utakayoyapata maana itafikia hata kuchubuliwa na kuwa na hali isiyotamanika mbele za watu. Mtumishi wa Mungu anapaswa kutoyajali hayo bali kujiweka daima katika utayari wa kuyatimiza mapenzi ya Mungu. Malipo yake ni furaha ya kumfanya Mungu aenee katikati ya wanadamu kwa maana Bwana asema: “kwa maarifa yake mtumishi wangu mwenye haki atawafanya wengi kuwa wenye haki; naye atayachukua maovu yao”.

Kristo anaielezea namna njema ya jinsi inavyopaswa utumushi wetu ili kuepukana na athari za kujitafutia malipo. Mitume watatu wanaomwendea kutafuta ukubwa wanaifunua hamu ya mitume wote na kwa kweli ni hamu ya binadamu wote. Mara zote tunaangaika, tunachuchumilia hali fulani na kujinidhamisha si kwa ajili ya utumumishi bali ni katika kutafuta ukubwa, utajiri na umaarufu. Kristo anatuambia: “mtu anayetaka kuwa mkubwa kwenu atakuwa mtumishi wenu, na mtu anayetaka kuwa wa kwanza wenu, atakuwa mtumwa wa wote”. Namna hii ni Mapinduzi makubwa kwa fikra na matamanio ya kibinadamu. Kristo anatuelekeza kujikita katika utumishi na kufanya ustawi wa watu wote bila kujishebedua mbele za watu.

Wale wanaojidai mbele za watu sababu ya utumishi wao au huduma yao bado wamesongwa na mkondo wa kidunia. Changamoto inayoambatana na utumishi unaoangalia katika malipo binafsi na si katika kuustawisha ufalme wa Mungu katikati ya wanadamu huonekana sana katika uzembe na kuchakachua kile mmoja anachoitiwa. Tabibu atashindwa kutekeleza vema kazi yake kama atachagizwa na hali hiyo, hali kadhalika na wahudumu wengine wa kijamii. Hapa ndipo tunaona athari zake kwa watoa huduma wengi kupenda kukimbilia kutoa huduma za kibinadamu mijini na sehemu “zinazolipa” na kuwaacha wale walio makabwela wakipambana na hali zao. Tujiulize, ndugu zetu hao tunaowaacha si binadamu ambao wewe umewekwa katika karama yako uliyopewa ili kuyafanya mapenzi ya Bwana kutimia mikononi mwako?

Maovu mengi dhidi ya binadamu yanayosababishwa na utumishi wa kujitafuta yanapata mwarobaini katika kenosi ya Kristo. Namna yake inakuwa njema zaidi kwani haishii kutufundisha tu bali yeye mwenyewe anatenda kwa mfano: “Kwa maana Mwana wa Adamu naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika na kuitoa nafsi yake iwe fidia ya wengi”. Kama anavyoelezewa katika somo la kwanza anapoteza kabisa haiba yake ya kimungu na inakuwa vigumu katika jicho la kawaida la kibinadamu kuuona umungu katika sura ya huyu anayeelezewa na Nabii Isaya. Kenosi yake ambayo inatufunulia maana ya unyenyekevu inajenga msingi wa utumishi unaoyapatia kipao mbele mapenzi ya Mungu na hivyo kujiepusha na ubinafsi wa kibinadamu. Ni hali ya kuwa tayari kuyaachia yote ili mwisho pamoja na wote uyapate yote.

Mtumishi wa somo la kwanza tunaambiwa kuwa “ataona mazao ya taabu ya nafsi yake, na kuridhika”. Hii inatupatia jambo jingine muhimu la kutafakari. Utumishi huu hata kama unapitia katika hali ya mateso kibinadamu, hata kama inaonekana kupoteza kibinadamu lakini si jambo la kupita bure tu. Kwa hakika linatupeleka katika matokeo chanya ambayo ni wokovu wa watu wote. Dominika iliyopita Kristo alithibitisha hilo kwa kuahidi kwamba yeye anayeacha vyote kwa ajili ya Kristo na kwa ajili ya Injili “atapewa mara mia sasa wakati huu… na katika ulimwengu ujao uzima wa milele”. Namna hii ya kuwa tayari kujiachia nafsi yako inahitaji ujasiri na masaada wa neema ya Mungu. Hivyo ukaribu wa vyanzo vya neema unapendekezwa ili kuepukana na vishawishi na tamaa za kidunia ambazo katika ujumla zinaiharibu haiba ya binadamu na kuathiri undugu kati yao.

Namna hiyo ya utumishi inayopendekezwa na Kristo inatufunulia upendo wa Utatu Mtakatifu sana. Upendo huo ambao umemwilika katika nafsi ya Kristo unamiminwa ndani mwetu na hivyo kuwa chanzo cha undugu wetu wa kibinadamu. Dhambi ya kwanza iliuondoa upendo huo na hivyo kumsambaratisha mwanadamu. Hapa tunaweza kuiona dhana ya dhambi kama hali ya mwanadamu kujitafutia mambo yake bila kuwa na Mungu wala kumtazama mwenzake aliye karibu yake. Dhambi inauharibu umoja kati ya mtu na muumba wake na kati yake na binadamu wenzake. Hivyo Kristo anatuelekeza kuufuata mfano wake wa unyenyekezu ili kuufunua na kuudhihirisha upendo huo wa Utatu Mtakatifu ambao ni ushindi dhidi ya dhambi.

Kristo Kuhani wetu mkuu anatufulia upendo huo kwa kuwa tayari kuitoa nafsi yake. “Yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi”. Yeye aliichukua namna yetu ya kibinadamu na akaonesha ushindi wa upendo wa Mungu ndani mwetu dhidi ya dhambi. Alipoungana nasi katika hali yetu ya kibinadamu aliibeba hali hiyo katika udhaifu wake wote, yaani, ukomo wetu na woga wetu ambao ulichagizwa na hali ya dhambi na kuturudisha katika wokovu kwa ushindi wa fumbo la Pasaka. Ndani ya ubinadamu wetu Kristo alirudisha tena uaminifu mkamilifu na usiotetereka kwa Mungu na hivyo kuwa kielelezo cha upya wa ubinadamu wetu. Namna hiyo inamfanya kuwa kweli kuhani wetu, yaani kiunganishi chetu sisi binadamu na Mwenyezi Mungu.

Hivyo tuitambue njia hiyo tunayoelekezwa na Kristo kwa kujikita katika utumishi unanuia kuustawisha utawala wa Mungu katikati ya wanadamu. Hiyo ndiyo tuzo kubwa tunayopaswa kuichuchumilia, yaani kumleta Mungu na kufanya watu wote na viumbe wote wauonje uwepo wake. Ushindi na malipo yetu yanawezeshwa na mfano wa Kristo anayetufundisha kati unyenyekevu wake ambapo ametuonesha kuwa tayari kuyaacha yote ili mwishoni kuyapata yote katika Mungu. Tuombe neema ya Mungu ili tupate ujasiri wa kujivika unyenyekevu wa Kristo.

J29 ya Mwaka
19 October 2018, 15:53