Familia ya Mama Teresa wa Calcuta waadhimisha sikukuu!
Frt. Titus Kimario - Vatican
Katika sikukuu ya Mtakatifu Mama Teresa wa Calcuta, “familia ya Mama Teresa” ilikutana kwa ajili ya misa ya kumkumbuka Mama Teresa na sala mbele ya kaburi lake katika nyumba mama ya Wamisionari wa Upendo. Askofu Mkuu Thomas D’Souza , aliongoza ibada ya Misa kunako saa 6.00 asubuhi masaa ya mahalia ambapo kulikua na mapadre zaidi ya 30 wa Mwili wa Kristo ambao walishirikiana naye ambalo ni shirika la kiume lililoanzishwa na Mama Teresa.
Baada ya misa, mapadre na waumini walikusanyika kuzunguka kaburi la Mama Teresa, Mama mkuu wa masista, Sista Mary Prema alikumbushia umuhimu wa kukaa kama familia. “Masikini, wasiopendwa na wasiotakiwa hawana familia. Mungu ametuchagua sisi kuwa familia yao. Watawa wote wa Mama Teresa, mabrother, mapadre na masista tumeitwa katika familia hii moja ili kuwa familia kwa ajili ya masikini”. Aliendelea kufafanua kwamba, sisi sote tumeitwa kushirikishana upendo wa Mungu katika roho ya furaha ya Mama Teresa. Sista Prema pia aliwasha mishumaa mitano katika kaburi la Mama Teresa, kama ishara ya matawi matano ya wamisionari wa Upendo wanaofanya kazi pamoja kama familia moja ya masista, mapadre, mabruda, walei wa kujitolea na wagonjwa.
Tangu siku ya kifo chake, 5 Septemba 1997 na baada ya mazishi ya kitaifa kama heshima kwake, kaburi la Mama Teresa ni kituo cha hija ulimwenguni kwa wakristu na hata watu wa imani nyingine. Papa Fransisko alimtangaza Mama Teresa kuwa mtakatifu mwishoni mwa mwaka wa huruma ya Mungu tarehe 4 Septemba 2016. Kwa watu waliokuwa wamemfahamu wanamshuhudia Mama Teresa kwamba alikua mtakatifu katika maisha yake.